Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dk Agnes Kijazi
MAMLAKA ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), imetoa hadhari ya kunyesha kwa mvua kubwa kuanzia kesho hadi mwisho wa mwezi huu, itakayosabaishwa na kimbunga kiitwacho Fantala.
Kimbunga hicho kipo katika eneo la Bahari ya Hindi kikienda kwa mwendo wa pole pole na kilikuwa hakijaleta madhara, lakini kwa sasa athari zake zimeanza kuonekana.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dk Agnes Kijazi alisema wanatarajia kuanzia kesho hali ya mvua itaendelea kuongezeka katika maeneo ya Ziwa Victoria na maeneo ya Magharibi.
Alisema kutokana na upepo kuvutwa na kimbunga hicho kwenda baharini, eneo kubwa la nchi litakuwa na mvua kubwa hivyo, wananchi wametakiwa kuchukua hadhari “Sasa tuko katika msimu wa mvua za masika, lakini kimbunga hiki kitasababisha ongezeko la mvua, hivyo ni vizuri tahadhari zikachukuliwa,” alisema.
Alisema tatizo kubwa la kimbunga hicho ni mgandamizo mdogo wa hewa unaoweza kuvuta upepo kutoka maeneo mbalimbali kwenda sehemu ambazo kimbunga kipo. Dk Kijazi aliongeza kuwa, kila siku wakati wa kutoa utabiri, watatoa tahadhari ya maeneo yatakayoathirika zaidi hivyo wananchi wanapaswa kuzingatia utabiri wa kila siku.
Alisema vimbunga vimekuwa vikipewa majina na nchi zilizo Ukanda wa Pwani ambayo hupendekeza kwa kufuata mpangilio wa herufi kulingana na msimu unaoanza Novemba mpaka Aprili na hiki ni kimbunga ni cha sita, lakini siyo vyote vyenye madhara kwa nchi.
Alisema vingine havijasikika kutokana na kutokuwa na madhara kwa nchi, lakini Fantala kina madhara ya kusababisha kuongezeka kwa mvua katika maeneo mengi ya nchi.
“Mpaka sasa tupo kwenye msimu wa mvua za masika zinazoendelea kunyesha na kuna dalili zinazoonesha kimbunga hicho kimeanza kuleta athari lakini kuanzia Jumapili na mvua zitaongezeka zaidi,” alisisitiza.