Serikali ya Uganda inafanya utathmini ambao huenda ukapelekea kutolewa kwa majeshi ya nchi hiyo nchini Somalia na Jamhuri ya Afrika ya Kati.
Msemaji wa jeshi la nchi hiyo Luteni Kanali Paddy Ankunda ameambia BBC kwamba kamati maalum imeundwa na mapendekezo yake yatafuatwa.
Hii si mara ya kwanza kwa serikali ya nchi hiyo kufanya utathmini wa majeshi yake yaliyo nchini Somalia na CAR lakini ni mara ya kwanza kwa wazo la kuondoa majeshi kutafakariwa.

Mdokezi wa kuaminika, ambaye hakutaka jina lake litajwe, ameambia BBC kwamba Rais Yoweri Museveni alikuwa amewazungumzia mabalozi wa kigeni kuhusu uwezekano wa majeshi ya Uganda kutolewa katika mataifa hayo mawili karibuni.
Uganda imechangia wanajeshi zaidi ya 6,000 katika kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa Afrika nchini Somalia (Amisom).
Wanajeshi hao wamekuwa wakisaidia kukabiliana na wapiganaji wa Kiislamu wa al-Shabab na kusaidia serikali ya Somalia.
Kikosi hicho huungwa mkono na Marekani na Umoja wa Ulaya.
Wanajeshi wa Uganda ndio wengi katika kikosi cha Amisom.