Mbunge wa Kawe, Halima Mdee.
MBUNGE wa Kigoma Mjini, Kabwe Zitto (ACT-Wazalendo) na wenzake wawili, jana wamehojiwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Haki, Kinga, Maadili na Madaraka ya Bunge, George Mkuchika kwa kufanya fujo bungeni kuhusu suala la Bunge kutorushwa ‘live’.

Mbali na Zitto, wengine waliohojiwa ni pamoja na Mbunge wa Kawe, Halima Mdee (Chadema) na Mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche (Chadema). Wabunge hao walihojiwa kwa tuhuma za kufanya fujo bungeni wakati ilipotolewa hoja ya Bunge kutorushwa moja kwa moja ‘live’, akiwa pamoja na wabunge wawili; Mdee na Heche.
Chanzo cha uhakika kutoka ndani ya kamati hiyo, kimesema Zitto alihojiwa na kamati hiyo kwa muda wa zaidi ya saa moja kwa makosa mbalimbali, ikiwamo kufanya fujo bungeni Januari 27, mwaka huu.
Taarifa hizo zilieleza kuwa Zitto alifanya fujo hizo baada ya Mwenyekiti wa Bunge, Andrew Chenge, kuahirisha kujadili hoja ya serikali iliyowasilishwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye, kuhusu Bunge kutorushwa ‘live’.
Hatua hiyo inatokana na hoja iliyowasilishwa na Zitto aliyetaka kuahirishwa kujadili hotuba ya Rais kutokana na kauli ya Waziri Nape ya kutorushwa matangazo ya moja kwa moja ya Bunge.
Zitto, alihojiwa na kamati hiyo ya Mkuchika kwa kilichoelezwa alisimama na kuomba mwongozo kuhusu jambo ambalo limekwishatolewa uamuzi kinyume na Kanuni ya 72 (1) na 68 (10 ya Kanuni za Kudumu za Bunge toleo la Januari 2016.
Mbali na hilo pia anadaiwa kusimama na kuzungumza bila utaratibu kinyume na Kanuni ya 60 (2) na 12 ya Kanuni za Kudumu za Bunge, jambo ambalo lilileta fujo na kuvunja shughuli za Bunge.
Katika barua za mwito zilizosainiwa na Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashilillah, Mei 12, mwaka huu, inaelezwa kwamba pamoja na mambo mengine na Mwenyekiti wa Bunge kumsihi mbunge huyo bado aliendelea kuzungumza na kusimama ikiwa ni kuonesha dharau kwa mamlaka ya Spika na shughuli za Bunge kinyume na kifungu namba 24 (d) na (e) cha Sheria ya Kinga na Haki za Bunge.
Barua hiyo ilieleza kuwa kutokana na vitendo hivyo vinavyokiuka Sheria ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge, Sura namba 296 na Kanuni za Bunge, wabunge hao walionywa kuwa endapo wasingefika mbele ya kamati hiyo jana hatua za kisheria zingechukuliwa dhidi yao kwa mujibu wa kifungu cha 15 na 31 (1)(a) na sheria ya Kinga, Madaraka na Haki za Bunge.