Rais wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amesema kuwa taifa lake linakusudia kufanya biashara na jamhuri ya Qatar haswa katika sekta ya gesi na usafiri wa ndege.
Rais Magufuli aliyasema hayo baada ya kukutana na balozi wa Qatar nchini Tanzania bwana Abdallah Jassim Al Maadadi.
Aidha rais Magufuli alitangaza nia ya kufungua ubalozi wa Tanzania mjini Doha kwa lengo la ''kuendeleza na kuimarisha zaidi uhusiano na ushirikiano na taifa hilo tajiri la ghuba.
"Najua Qatar ina uzoefu katika maeneo hayo na sisi Tanzania tungependa tushirikiane nanyi kuwekeza na kubadilishana uzoefu ili fursa hizo zilete manufaa kwa pande zote mbili" amesema bw Magufuli.

Image copyrightAFP
Image captionTZ yataka uzoefu wa Qatar sekta ya gesi

Katika taarifa kwa vyombo vya habari iliyotiwa sahihi na mkurugenzi wa mawasiliano wa ikulu Gerson Msigwa bw Magufuli alimtaka balozi huyo amhamasishe kiongozi wa Qatar , Sheikh Tamim bin Hamad Al Thani na Jumuiya ya
wafanyabiashara wa Qatar kuhusu ''fursa nyingi za ushirikiano zinayoweza kufanyiwa kazi, huku akibainisha uwepo wa gesi asilia zaidi ya futi za ujazo Trilioni 57 na mpango wa kufufua shirika la ndege la taifa (ATCL)''.