1Dar es Salaam
Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima amemjibu katibu mkuu wa zamani wa CCM, Yusuf Makamba aliyemtuhumu kuwa ni mwongo akisema leseni yake ni ya kuendesha magari makubwa na siyo vibajaji na maguta. 
Akihubiri katika kanisa lake jana, Gwajima bila kutaja jina la Makamba, alisema: “Siwezi kushughulika na vigari vidogovidogo nyie mnanifahamu, mimi nina leseni ya kuendesha semi trailer …nadhani mmenielewa,” alisema huku waumini wake wakimshangilia.
Juzi, Makamba aliwaeleza wajumbe wa Mkutano Mkuu Maalumu wa CCM kuwa Askofu Gwajima ni kiongozi wa dini lakini ni muongo na kuwa uongo wake unawaudhi hata waumini wake ambao ni wanachama wa chama hicho.
Alisema Gwajima amekuwa akisema uongo kuwa Rais mstaafu, Jakaya Kikwete hataki kuachia madaraka ya uenyekiti wa chama hicho, kitu ambacho Rais huyo mstaafu alikanusha akisema ni yeye alikwenda kumshawishi Dk John Magufuli kuchukua nafasi hiyo kabla ya muda wa uliopangwa kikatiba.
Katika mahubiri hayo, Gwajima pia alisema mafunzo aliyoyapata tangu akiwa mdogo ni kuogopa kugombana na watu wa aina tatu, walevi, wazee na wagonjwa.
“Baba yangu alinifundisha nisigombane na walevi, wazee na wagonjwa kwani ukimpiga kidogo mtu wa aina hiyo anaweza kufa,” alisema Gwajima.
“Hata nyie waumini wangu nawaomba msigombane na watu wa aina hiyo kwani mnaweza kupata matatizo,” alisema.
Kiongozi huyo aliongoza mamia ya waumini wake kumuombea Rais Magufuli kwa kushinda uenyekiti wa CCM akisema kofia hizo mbili zimempa meno ya kung’ata na zitamwongezea kasi ya kutatua matatizo ya wanyonge nchini.
Rais Magufuli juzi alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa CCM baada ya kupata kura zote 2,398 alizopigiwa na wajumbe wa mkutano huo.
Kutokana na ushindi huo, Gwajima alisema Magufuli amepewa meno ya `kung’ata’ kila upande tofauti na alipokuwa na kofia moja ya urais.
Alisema kwa muda mfupi aliokaa madarakani, elimu ya msingi na sekondari zimeanza kutolewa bure kitendo ambacho maskini na wanyonge wa nchi hii wameanza kuuona mwanga.
Alisema ataendelea kumwombea Magufuli kwa sababu kazi anazozifanya zinawanufaisha wanyonge na maskini ambao kwa muda mrefu walipuuzwa katika nchi yao.
“Kuchaguliwa kwake kuwa mwenyekiti ni zawadi kwetu Watanzania, tuendelee kumwombea kila siku ili aendelee kufanya kazi yake kwa ufanisi zaidi,” alisema.
Alisema nafasi hiyo mpya itamwezesha kupambana na rushwa tatizo ambalo ameonyesha kuwa `atalivalia njuga’ hata ndani ya chama hicho.
Mbali na Rais Magufuli, Gwajima aliwaombea pia Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, mawaziri na Spika wa Bunge kwamba Mungu awalinde ili wamsaidie Rais kutekeleza majukumu yake.
Kwa mwezi mzima, Askofu Gwajima amekuwa akitafutwa na Polisi baada ya kusambaa kwa sauti inayosikika kama yake ikitaka Rais mstaafu Kikwete afikishwe mahakamani kwa makosa yote yaliyofanyika katika utawala wake.
Katika mkanda huo, sauti hiyo inadai baadhi ya viongozi wa CCM wametuma watu mikoani kupiga kampeni ya kutaka Magufuli asipewe uenyekiti ambao umekuwa ukishikiliwa na Kikwete.
Baada ya sauti hiyo, Gwajima aliondoka nchini kwenda Japan lakini Polisi waliendelea kumsaka hadi Julai 12 walipomkamata katika Uwanja wa Mwalimu Julius Nyerere (JNIA), aliporejea. Alihojiwa na kuachiwa siku hiyohiyo.