Wakuu katika maeneo ya Kusini mwa Ujerumani, wamesema kuwa mtu mmoja amejilipua ndani ya baa na kuwajeruhi watu wengine 12, watatu kati yao vibaya sana.
Maafisa wa serikali wanasema mshukiwa ni raia wa Syria ambaye alikuwa ameshindwa kupata hifadhi nchini Ujerumani mwaka jana.

Mlipuko huo ulitokea katika mji wa Ansbach karibu na tamasha moja la muziki ambalo ni maarufu sana katika eneo hilo.
Zaidi ya watu elfu mbili wameondolewa kutoka katika tamasha hilo, ambalo baadaye lilisitishwa. Baadhi ya maeneo ya mji huo wa Ansbach, yamezingirwa na walinda usalama.
Ni shambulio la tatu huko Bavaria, katika kipindi cha wiki moja.
Ijumaa, watu tisa walifariki shambulio la ufyatuaji risasi mjini Munich na siku chache awali, kijana aliwashambulia watu kwa kisu na shoka kwenye treni.