JESHI la Polisi mkoani Dodoma limepiga marufuku na kuwataka wananchi wasishiriki katika maandamano ya Septemba mosi mwaka huu.
Limesema maandamano hayo ya Ukuta, yanayoandaliwa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), si halali na yana nia ovu ya kuvuruga amani na utulivu wa nchi.

Katika mkutano wake na waandishi wa habari leo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Lazaro Mambosasa amesema kwa muda mrefu kumekuwa na makundi ya wafuasi wa Chadema, kuhamasishana ili kufanya vurugu kupitia hoja ya maandamano waliyoyapa jina la UKUTA.
"Wapo watu wanaosambaza machapisho mbalimbali yenye kauli za uchochezi katika fulana , mabango na katika mitandao ya kijamii, pia wapo wanofanya kampeni zisizo halali nyumba kwa nyumba kushawishi watu kufanya uhalifu huo," alisema.