Wanachama wa tume ya Uchaguzi mkuu nchini Gabon wametangaza kuwa rais Ali Bongo, amehifadhi kiti chake cha urais baada ya kumshinda mpinzani wake Jean Ping.
Ushindi huo ni baada ya kumalizika kwa shughuli za upigaji kura, hapo siku ya Jumamosi.

Lakini mwaandishi wa habari wa BBC mjini Libreville, amesema kuwa wajumbe wanaowakilisha upinzani katika tume ya uchaguzi, wameondoka ndani ya ukumbi wa kuhesabu na kusawazisha matokeo ya kura, na kukataa kutia saini hati zinazompa ushindi rais Bongo.
Walinda usalama wanapiga doria katika barabara za mji mkuu Libreville huku taharuki ikitanda kote nchini humo.
Familia ya Bongo imetawala Gabon kwa nusu karne huku Omar Bongo akitawala kwa miongo minne, na mwanawe rais wa sasa Ali, alichukua hatamu za uongozi mnamo mwaka wa 2009.