David Kafulila
KWA mara nyingine tena Mahakama imetupa maombi ya kupinga matokeo ya uchaguzi yaliyofunguliwa na David Kafulila akipinga ushindi wa Husna Mwilima wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Jimbo la Kigoma Kusini, safari hii uamuzi ukitolewa na Mahakama ya Rufaa.

Katika uamuzi uliotolewa jana na jopo la majaji watatu wa Mahakama ya Rufaa chini ya uenyekiti wa Jaji Mbarouk Salim akisaidiwa na Jaji Bernard Luanda na Jaji Richard Mziray, mahakama hiyo imetupilia mbali rufaa hiyo ya Kafulila kwa kile ilichodai imekosa miguu ya kusimama.
Mbali ya uamuzi huo, jopo hilo la majaji wa Mahakama ya Rufaa pia limemtaka mlalamikaji ambaye hawakuwepo mahakamani kulipa gharama za shauri hilo la madai namba 212/2016.
Majaji hao walisema wanakubaliana na maombi ya Wakili wa Serikali Gabriel Mallata aliyepinga shauri hilo kusikilizwa kutokana na kile alichodai kwamba halikukidhi matakwa ya sheria.
Hii ni mara ya pili kwa Kafulila kuangushwa kisheria katika shauri alilofungua kupinga ushindi wa mgombea wa CCM Mwilima ambaye ndiye Mbunge halali wa Jimbo la Kigoma Kusini, mara ya kwanza ikiwa ni Mei, mwaka huu, shauri lake lilitupwa na Jaji Ferdnand Wambali wa Mahakama Kuu aliyesikiliza shauri mama.
Kafulila katika rufaa yake kwa Mahakama ya Rufaa alikuwa akidai kuwa Jaji wa Mahakama Kuu aliyesikiliza shauri lake hakumtendea haki kwa kumnyima ushindi aliostahili.
Hadi kufikia hatua hiyo, shauri hilo ndilo ambalo limesikilizwa na majaji wengi tangu lilipoanza. Katika hatua ya awali pekee lilisikilizwa na majaji watatu tofauti wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora.
Miongoni mwa majaji waliosikiliza shauri hilo ni Jaji John Utamwa, Leila Mgonya na Sam Rumanyika ambaye alikamilisha usikilizaji wa awali na baadaye likapangiwa kwa Jaji Wambali.