KIWANDA cha Uzalishaji Sukari cha TPC Ltd cha wilayani Moshi mkoani Kilimanjaro, kimeitikia ombi la Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kwa kutoa msaada wa Sh milioni 20 kwa wananchi wa Mkoa wa Kagera waliokumbwa na maafa ya tetemeko la ardhi Septemba 10, mwaka huu.

Msaada huo umelenga familia ambazo zimepata majanga hayo huku pia baadhi ya taasisi zikiwamo za elimu, afya, dini na miundombinu mingine ambayo imeathiriwa na tetemeko hilo.
Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Saidi Mecky Sadiki alisema jana kuwa msaada huo unafanya fedha zilizotolewa na mkoa huo kwenda Kagera kuwa Sh milioni 127.
“Kimsingi hapakuwa na mashindano ya kutoa fedha lakini kama waungwana na kuonesha umoja wa kitaifa, tuliguswa kama mkoa kuwasaidia Watanzania wenzetu wa mkoa wa Kagera Sh milioni 127,” alisema Sadiki.
Akizungumza na watumishi wa Wilaya ya Siha, Sadiki alisema kiasi kilichotolewa na TPC kimetumwa mkoani Kagera kwani hapo awali tayari serikali ya mkoa ilishawasilisha mchango kwa wakazi wa Kagera.
"Michango yote ya mkoa wa Kilimanjaro imeonesha jinsi tulivyo na ushirikiano kuanzia mashirika binafsi, taasisi za dini, wafanyabiashara wakubwa na wadogo, wananchi na watumishi, ninawashukuru,” alisema.
Katika hatua nyingine, baadhi ya watumishi wa halmashauri hiyo walilalamikia kukosa usafiri wa uhakika wa kwenda na kurudi kazini baada ya kutokuwapo kwa daladala kutokana na barabara mbovu.
Mganga wa Mifugo wa Wilaya, Dk Barnabas Mbwambo aliomba serikali kutoa fedha za bajeti kwa wakati kwani tangu kupitishwa kwa bajeti Julai mwaka huu, bado fedha hazijafika wilayani, jambo linalosababisha wao kushindwa kwenda vijijini kuhudumia wananchi.