Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, Monica Mnanka (kushoto), akizungumza na waandishi wa habariwakati akimkaribisha msajili wa vyama kuzungumza na wanahabari Dar es Salaam leo asubuhi. Kulia ni Msaji Msaidizi wa Vyama vya Siasa, Sisty Nyahoza na Msajili wa Vyama, Jaji Francis Mutungi.
 Msajili wa VVyama vya Siasa nchini, Jaji Francis Mutungi (kushoto), akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Dar es Salaam leo, wakati akitoa taarifa ya kufutwa kwa usajili wa kudumu wa vyama vitatu vya siasa ambavyo ni Chama cha Haki na Ustawi (Chausta), chama cha The African Progressive Party of Tanzania (APPT Maendeleo) na Chama cha Jahazi Asilia. Kulia ni Msajili Msaidizi, Sisty Nyahoza.
 Mkutano na wanahabari ukiendelea.
Wanahabari wakichukua taarifa hiyo.

Na Dotto Mwaibale

MSAJILI wa Vyama vya Siasa nchini Jaji Francis Mutungi kwa mamlaka aliyonayo chini ya kifungu cha 19 cha Sheria ya vyama vya Siasa namba 5 ya mwaka 1992, amevifutia usajili wa kudumu vyama vitatu vya siasa kuanzia leo hii.

Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari ofisini kwake leo asubuhi Jaji Mutungi alivitaja Vyama alivyovifuta kuwa ni Chama cha Haki na Ustawi (Chausta), kilichopata usajili wake Novemba 15, 2001 kilichokuwa kikiongozwa na James Mapalala kama Mwenyekiti wa Taifa na Mwaka Lameck Mgimwa kama Katibu Mkuu.

Chama kingine alichokifutia usajili wa kudumu ni Chama cha The African Progressive Party of Tanzania (APPT Maendeleo)  kilichopata usajili Machi 4, 2003 kilichokuwa kikiongozwa na Peter Kuga Mziray kama Rais Mtendaji Taifa na Nziamwe Samwel kama Katibu Mkuu.

Jaji Mutungi alikita chama kingine alichokifuta kuwa ni  Chama cha Jahazi Asilia kilichokuwa kikiongozwa Kasimu Bakari Ally kama Mwenyekiti wa Taifa na Mtumweni Jabir Seif kama Katibu Mkuu ambacho kilipata usajili wa kudumu Novemba 17, 2004.

Mutungi alisema vyama hivyo vimepoteza sifa za usajili wa kudumu kwa kukiuka masharti ya Sheria ya Vyama vya Siasa, ambapo kila chama klipewa taarifa ya nia ya Msajili wa Vyama vya siasa kufuta usajili wake wa kudumu na kutakiwa kueleza kwanini kisifutwe ambapo vilishindwa kutoa sababu za kuridhisha kuwa havikukiuka sheria na bado vinavyo sifa za usajili wa kudumu.