Kiungo wa kati wa Chelsea Eden Hazard ameumia katika kifundo cha mguu wake wa kulia akiwa mazoezini na timu ya taifa, Shirikisho la Soka la Ubelgiji limesema.

Maafisa wa RBFA wameandika kwenye Twitter kwamba kiungo huo aliumia na baada ya kupimwa ikabainika alikuwa amevunjika mfupa kidogo.
Mchezaji huyo wa miaka 26 sasa atakosa mechi ya kirafiki ya Ubelgiji dhidi ya Jamhuri ya Czech na mechi ya kufuzu kwa Kombe la Dunia dhidi ya Estonia tarehe 9 Juni.
Haijabainika atarejea lini kucheza.
Hazard alisaidia sana Chelsea kushinda Ligi ya Premia msimu uliomalizika majuzi, ambapo aliwafungia mabao 16 katika mechi 36.
Amesalia na miaka mitatu katika mkataba wake Stamford Bridge, lakini kuna taarifa ambazo zimekuwa zikimhusisha na kuhamia Real Madrid.