Mshambuliaji wa Barcelona Lionel Messi amesema angependa kusalia na klabu yake kwa siku zilizosalia katika taaluma yake.
''Ni kitu ambacho nimekuwa nikikitazamia na ni kitu nilichokuwa nikikitaka," alisema.

Kiungo huyo wa Argentina mwenye umri wa miaka 29 alijiunga na Barcelona akiwa na umri wa miaka 13, akashiriki mechi yake ya kwanza akiwa na umri wa miaka 17 na amefunga zaidi ya magoli 500 akiwa na klabu hiyo.
Messi ameshinda taji La liga mara nane, Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya mara nne na tuzo mchezaji bora duniani Ballon d'Or mara tano.
Msimu uliopita chini ya kocha Luis Enrique, Barcelona walikuwa katika nafasi ya pili kwa ligi ya La Liga, alama tatu chini ya mabingwa watetezi wa Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya Real Madrid.
Walishindwa 3-0 katika robo fainali Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya dhidi ya Juventus.
Enrique alitangaza mwezi Machi, kwamba angeiaga klabu hiyo baada ya mkataba wake wa miaka mitatu kumalizika, mechi yake ya mwisho ilikuwa ni pale Barca walipojinyakulia kombe la Copa Del Rey .
Messi alifunga bao la ufunguzi walipoichapa Alaves mabao 3-0 na kupata ushindi.
Messi ambaye alikuwa wa pili nyuma ya mshambuliaji wa Real, Cristiano Ronaldo katika tuzo ya Ballon d'Or, aliuambia mtandao wa Barcelona lengo lake ni ''kujaribu kuimarika kila msimu hadi mwisho, na hilo ndilo lengo langu la msimu ujao.''