Na Shakoor Jongo
DIVA wa filamu Bongo asiyekaukiwa na habari, Wema Sepetu juzikati alijikuta akiangua kilio hadharani na kuwaacha watu midomo wazi.
Tukio hilo la kushangaza lilijiri wikiendi iliyopita, ndani ya Ukumbi wa Nyumbani Lounge, Kinondoni, Dar kulipokuwa na muendelezo wa sherehe ya ‘Kichen Party’ ya Mtangazaji wa Runinga ya Star, Sauda Mwilima.
Mnyetishaji wetu aliyemng’ata sikio askari wa Risasi Mchanganyiko, alisema Wema alifikia hatua hiyo baada ya kupewa umbeya na msichana mmoja ambaye jina lake halikufahamika mara moja kuwa mpenzi wake Naseeb Abdul ‘Diamond’ yupo maeneo f’lani na Jokate Mwegelo.
Katika kusherehekea huko, Wema akiwa hana hili wala lile alionekana akinong’onezwa na mdada aliyekuwa naye jirani, haukupita muda mrefu, mambo yakaharibika.
Wema ambaye muda huo alikuwa amehamaki, alionekana akiangua kilio, kitendo kilichowafanya baadhi ya mastaa waliokuwa karibu naye wamwulize kulikoni. Jibu lililopatikana lilikuwa ni kapewa umbeya kuwa Diamond yupo na Jokate.
Mashostito zake waliingia mzigoni kuhakikisha Wema anatulia kwa kumwambia kwamba huenda maneno hayo si ya kweli.
“Wema acha kulia bwana, huyo aliyekuambia maneno hayo huenda kakudanganya tu, watu wambeya sana, sasa kakwambia hivyo ili iweje?” alihoji dada mmoja aliyekuwa karibu na Wema.
Baada ya kuambiwa maneno hayo, msanii huyo alipunguza munkari na kusema: “Naumia sana, nahisi nimeletwa duniani kwa ajili ya kuumizwa na mapenzi… ila ipo siku yataisha.”