Pichani ni baadhi ya  wachezaji wa timu zote na viongozi wao wakipata picha ya pamoja
Kikosi cha timu ya Antwerpen

Kikosi cha Veteran

Wachezaji wa veteran wakishangilia ushindi wao wa goli 5-3 dhidi ya Antwerpen

Jumamosi ya tarehe 14.5.2016 kulikuwa na mpambano kati ya Antwerpen Fc na wachezaji wazamani Veteran,mchezo uliochezwa jijini Antwerpen.
Wachezaji wa timu zote mbili waliingia uwanjani wakiwa na morali ya ushindi huku kila mmoja akiahidi ushindi kwa mwenzake.

Mpira ulianza kwa kasi huku timu ya Antwerpen ikiwa na wachezaji wake wadogo na wenye kasi ya mbio kwa kulisakama lango la wakongwe Veteran mfululizo ila uhodari wa golikipa wa Veteran Kuyala[kiduchu] aliweza kuyakabili vyema mashambulizi hayo.

Muzamilu ndiye aliyeanza kufungua ukurasa wa magoli kwa timu yake ya Veteran kunako dk ya 20 ya mchezo.Dk 15 baadae yani dk ya 35 Sele Rasta aliweza kuisawazishia timu ya Antwerpen.Muda mfupi baadae beki wa Veteran Abdulratif aliunawa mpira eneo la hatari na hivyo kuipa Antwerpen Fc bao lingine kwa njia ya penati lililofungwa kiustadi na Ronda.Mpaka mapumziko Antwerpen Fc 2-1 Veteran.

Kipindi cha pili kilianza vizuri huku kila timu ikijaribu kusawazisha makosa yake ila dakika ya 56 Veteran waliweza kusawazisha bao la pili kupitia mshambuliaji Jamal.Dakika nne baadae Veterani waliongeza bao la 3 baada ya mchezaji Mambo Tela kumuadaa golikipa Ndela kwa kufunga kiufundi mpira wa adhabu.

Jamal akiendeleza ufungaji kwa timu ya Veteran aliongeza goli la nne dakika ya 70 ya mchezo.Muda mfupi tena Ronda akaiandikia timu yake ya Antwerpen Fc goli la 3 kwa njia ya penati baada ya makosa yaliyofanywa na mmoja wa wachezai wa Veteran.Mpira ukiendelea kuwa mkali kila timu ikiwa na mashambulizi ya mara kwa mara ila Veterani walionyesha umahiri wa kulicheza kambumbu na kuwafundisha vilivyo soka vijana wa Antwerpen Fc.

Bahati haikuwa yao siku hiyo kwani Veterani waliendeleza dozi dakika ya 85 ya mchezo baada ya mchezaji matata Mambo Tela kuunganisha krosi kali ya Fouad na kuandika bao la 5 na la ushindi.

Mchezo ulikuwa mzuri na wa kusisimua.